SERIKALI NCHINI TANZANIA YAFUTA KODI YA PANGO LA ARDHI KWA MADHEHEBU NA TAASISI ZA DINI


SERIKALI Imefuta kodi ya pango la ardhi kwa Taasisi na Madhehebu ya dini nchini kuanzia mwaka wa fedha wa 2018/2019.

Hatua hiyo imetangazwa juzi Jumapili Januari 27, 2019 na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi jijini Mbeya wakati wa ibada ya kuwaweka wakfu viongozi wa Jumuiya Kuu ya Kanisa la Kibaptisti Tanzania (BCT).

Lukuvi amesema Rais Magufuli ameiagiza wizara hiyo kutoyatoza kodi madhehebu ya dini kwa sehemu ambazo zimeandaliwa kwa ajili ya kufanyia ibada.

"Rais ameagiza kuanzia Julai mosi mwaka huu wa fedha madhehebu ya dini yasilipe kodi ya ardhi kwa maeneo ambayo huduma za maombi na ibada zinatolewa, hata hivyo msamaha huu hauhusu maeneo ambayo kuna miradi ya kuingiza fedha ambayo tunajua madhehebu mengi yameanzisha," alisema Lukuvi.

Amesema maagizo hayo tayari yametolewa kwa makamishna wa ardhi wa kanda na mikoa pamoja na maofisa ardhi wa majiji, manispaa na halmashauri nchi nzima.

Hata hivyo, Lukuvi ametoa nafasi ya kukutana na viongozi wa dini ambao wana migogoro ya ardhi kwenye maeneo ambayo wanatoa huduma.

"Najua kuna migogoro mingi kwenye maeneo ambayo mnatoa huduma hivyo nawakaribisha ofisini kwangu Dodoma na kama migogoro itakuwa mikubwa nitafika mpaka eneo la mgogoro," alisema Lukuvi.


“Wizara yangu imepewa jukumu la kutatua migogoro ya ardhi kabla ya mwaka 2020 na tusipotatua migogoro ya dini inaweza kupelekea uvunjifu wa amani nchini hivyo hatutaki kuifuga migogoro iliyopo,” alisema.


Awali, askofu wa kanisa la Baptisti nchini, Arnold Manase amesema kanisa lake ni moja ya madhehebu yanayoongoza kuwa na migogoro ya ardhi na baadhi ya waumini wa kanisa hilo.

"Kwa kuwa waziri mwenye dhamana upo naomba nafasi nije ofisini kwako nikueleze migogoro iliyopo ndani ya kanisa langu ili uangalie namna ya kuitatua maana migogoro imekithiri mpaka kufikia hatua ya kujenga makundi miongoni mwa waumini," alisema Manase.

Share on Google Plus

About Jacktan Msafiri

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

Post a Comment